Saturday, January 26, 2013

Tambiko likiondoka



KAMA mbuyu na mkuyu, tambiko lilipokaa,

Watu huja kwa miguu, kuja soma zao dua,

Kafara wasisahau, mashinani kuzitoa,

Tambiko likiondoka, koo husambaratika !

 

Wazazi huyanukuu, mila zikafuatia,

Wakarithi wajukuu, na kizazi kwendelea,

Kwa gharama na nafuu, hakuna wa kuchimbua,

Tambiko likiondoka, koo husambaratika !

 

Wazima nao mafuu, kuuuliza hukataa,

Wakahofu ubahau, kizazi kutunukiwa,

Au ya koo dharau, na wengine kuchukia,

Tambiko likiondoka, koo husambaratika !

 

Lilipo ni sikukuu, hadi likijang'olewa,

Pakabaki kichuguu, mchwa kwenda kuhamia,

Yakaanza mahuruhu, makaburi kufagia,

Tambiko likiondoka, koo husambaratika !

 

Moyo wangu ni juzuu, hapa nilipofikia,

Hakijaja kitukuu, na sijaijua dunia,

Na sijda na rukuu, wala hazijatimia,

Tambiko likiondoka, koo husambaratika !

 

Si cha maji kitunguu, na saumu sijakuwa,

Nazihofu dafrau, za siasa na kuzua,

Naitafuta nafuu, penye ukiwa kukaa,

Tambiko likiondoka, koo husambaratika !

 

Nawaachia ukuu, waliobeba dunia,

Mimi naenda sahau, yote nikayaachia,

Nikahifadhi nahau, wajukuu kuzijua,

Tambiko likiondoka, koo husambaratika !

 

Namshukuru Afuu, hapo nilipofikia,

Mukubuli nanukuu, yake nimeyaridhia,

Naendeleza juzuu, daraja nende patiwa,

Tambiko likiondoka, koo husambaratika !

No comments: