Saturday, January 26, 2013

Nilinyanyua mkono


Sijui kilichokuwa, wala lililotokea,

Lengo sikukusudia, na shabaha haikuwa,

Naona kusalimia, na sio kusalimiwa,

Mkono nilinyanyua, wewe hukuangalia!

 

Tumekuwa ni sanaa, kucheka na kuchekua,

Na kisha wanaolia, sinema wakafanziwa,

Huruma sijaijua, ila ujinga kupewa,

Mkono nilinyanyua, wewe hukuangalia!

 

Naishangaa dunia, upuzi ilivyokuwa,

Kile cha kuwajalia, ndio kinadharauliwa,

Na hasara kilokuwa, ndio kinathaminiwa,

Mkono nilinyanyua, wewe hukuangalia!

 

Njia niliichagua, sisi sote kutembea,

Nyuma wewe ukakaa, kama unanitegea,

Njiapanda kufikia, kushoto ukaingia,

Mkono nilinyanyua, wewe hukuangalia!

 

Kamwe sikukuambaa, unyayo nikafatia,

Nilipokushuhudia, sikuacha kujitoa,

Kama ungeangalia, sura usingekosea,

Mkono nilinyanyua, wewe hukuangalia!

 

Ukubwa umekuoa, nasaba kuikataa,

Na marafiki wakiwa, hutaki kuwasikia,

Juu umejinyanyua, daraja kujitwalia,

Mkono nilinyanyua, wewe hukuangalia!

 

Sitaki kukuvamia, wala kukukaribia,

Ila ninashtakia, zamani ilivyokuwa,

Halali kama ni sawa,  Mola atakujalia,

Mkono nilinyanyua, wewe hukuangalia!

 

Chako sijakililia, wala ombaomba kuwa,

Uhusiano wa riha, sasa nimeutambua,

Ami hawajatokea, wa kweli waliokuwa,

Mkono nilinyanyua, wewe hukuangalia!

No comments: