CHA mkonokitambaa, machozi ulofutia,
Mimi nilikichukua, na sasa nakitumia,
Machozi kujiuftia, kwa wewe kuondokewa,
Hanky
-yo, bado ninayo, najifutia machozi!
Marashiyo yanukia, kama vile yanalia,
Na poda uliyotia, kikohozi yanitia,
Kila nikijiwazia, kosa langu sijajua,
Hanky
-yo, bado ninayo, najifutia machozi!
Ufukara nakisia, waweza ukachangia,
Njaa ninayonukia, rahisi kuifichua,
Wewe ulipogundua, hukuweza vumilia,
Hanky
-yo, bado ninayo, najifutia machozi!
Kwaheri hukuitoa, wala kunisimbulia,
Njia uliichagua, ifaayo kufatia,
Upweke kuniachia, mwenye nacho kujaliwa,
Hanky
-yo, bado ninayo, najifutia machozi!
Ila ninachokijua, langu kweli lilikuwa,
Mizanini ungetia, zana ingelizubaa,
Kwa upande kuzidiwa, hadi chini kugotea,
Hanky
-yo, bado ninayo, najifutia machozi!
Moyo nilikuachia, upate kupalilia,
Bustani kuchanua, mengine yangefatia,
Haraka uliyokuwa, hukuweza jizuia,
Hanky
-yo, bado ninayo, najifutia machozi!
Kuishi ulihilakiwa, mapema kutangulia,
Fisadi kumkimbilia, idadi asiyewajua,
Silaani, ninakwambia, hilo utalijutia,
Hanky
-yo, bado ninayo, najifutia machozi!
Ya kweli umeachia, ukafata ya kuzua,
Yaliyojaa sanaa, ukweli zisizokuwa,
Laiti ningelijua, nisingelikuangalia,
Hanky
-yo, bado ninayo, najifutia machozi!
Laiti ningelijua, nisingelikuangalia,
Machowe yalolegea, ukawa wanilogea,
Nami sikujitambua, na ukweli kuujua,
Hanky
-yo, bado ninayo, najifutia machozi!
No comments:
Post a Comment