Wednesday, January 16, 2013

Watu wakishaamka


Kushoto umeptia, kulia ungegeukia,

Hali ukaitambua, na vyanzo kuvielewa,

Haraka ukitumia, mguu utaumia,

Watu wakishaamka, wape kazi wakafanze !

 

Watu wajiamkia, maji ni kuwapatia,

Uso wapate kunawa, tongotongo kuondoa,

Na njia ya kufungua, kwanza kuwasalimia,

Watu wakishaamka, unawapa blanketi ?

 

Vitisho wamezoea, tangia ya kuzaliwa,

Hadi mamba watumiwa, na simba akafatia,

Hofu walishaivua, hasira imebakia,

Watu wakishaamka, wape kazi wakafanze !

 

Jua wanajionea, chiniye yanayotokea,

Giza wala halijawa, vipi unafikiria,

Na hesabuu wazijua, waweza kukutajia,

Watu wakishaamka, unawapa blanketi ?

 

Staftahi wangojea, weye wawakoromea,

Na mgeni alokuwa, siye wao, wakujua,

Heshima ukikosea, nani nguo ajivua ?

Watu wakishaamka, wape kazi wakafanze !

 

Sheria hujadumaa, haki isipoijua,

Dhuluma ikandaiwa, na mengi kusingiziwa,

Na mikuki kutupiwa, kila inapotokea,

Watu wakishaamka, unawapa blanketi ?

 

Kuteta ni kufikiria, wala si jambo kuzua,

Neno lisipoangaliwa, vita laweza kuzua,

Haki ikibaguliwa, huja ngao ikavaa,

Watu wakishaamka, wape kazi wakafanze !

 

Mambo yataka hatua, nyumbani yakabakia,

Hadharani kutotoa, chunguni yanapokuwa,

Au wote tutakuwa, nasi ni watuhumiwa,

Watu wakishaamka, unawapa blanketi ?

 

Ugaidi  mwanunua, kwa faida kutumia,

Ya kwenu kujijengea, hali ya umma yapwaya,

Kila mwenye kuyajua, uongo huugundua,

Watu wakishaamka, wape kazi wakafanze !

 

Yabadilika dunia, kadhalika Tanzania,

Hakuna aliyepewa, hatimilki kutwaa,

Yake kujiamlia, jinsi anavyojisikia,

Watu wakishaamka, unawapa blanketi ?

 

No comments: