Saturday, January 26, 2013

Wewe ukishakipata

 
Ndivyo ilivyo dunia, watu huipigania,
Na wanachopigania, hamu ikawaishia,
Wakishakujipatia, tafrani zikapoa,
Wewe ukishakipata, changamoto hupotea!
 
Husumbuka na dunia, bilkuli kuwania,
Kwa linalowazuzua, mfukoni kulitia,
Hamadi likitulia, ari inadidimia,
Wewe ukishakipata, changamoto hupotea!
 
Mbio watazitimua, nyikani wakapotea,
Marathoni mara kuwa, ovyo wanajihemea,
Ila wakiambulia, hurudi wakatulia,
Wewe ukishakipata, changamoto hupotea!
 
Hutamani ya dunia, na wao kujipatia,
Mikononi wakitia, hawa inawaishia,
Jingine kuangalia,wapi la kulifuatia,
Wewe ukishakipata, changamoto hupotea!
 
Hutetemesha jamaa, hadi wakamchukia,
Na dharau kuzitoa, vishindo akavitia,
Akatingisha dunia, tunda kwenda liangua,
Wewe ukishakipata, changamoto hupotea!
 
Likija mdondokea, kudaka huparamia,
Kisha akachuchumia, mikononi kulitia,
Anapoliangalia, si dhahabu akajua,
Wewe ukishakipata, changamoto hupotea!

No comments: