Kinaweza kupotea, tena
kutokujionea,
Ukabakia mkiwa, daima wewe kulia,
Na kurudi sio njia, huyoyoma na
kwishia,
Unachokitegemea, kinaweza
kupotea!
Leo unakiringia, kesho
utakililia,
Kisha ukaugilia, asante hukuitoa,
Shere ulikichezea, na dosari
kukitia,
Unachokitegemea, kinaweza
kupotea!
Ujivuni ukavia, na kukushuka
kifua,
Haya ukaisikia, wengi
ulivyonyanyapaa,
Ukajuta kwa kinaya, tena
hutojionea,
Unachokitegemea, kinaweza
kupotea!
Wote uliowaambaa, hutamani
kurejea,
Na wasiojitambua, mtego
wataingia,
Ila kwa wenye kujua, mbali sana
watakaa,
Unachokitegemea, kinaweza
kupotea!
Nafasi hukuachia, upate vema
pumua,
Njia wakaifagia, pasina kuitumia,
Milango wakifungua, ndani patupu
pakawa,
Unachokitegemea, kinaweza
kupotea!
Macho watayachezea, kama
makengeza kuwa,
Na duara kuyatia, kama Kipanya
wakawa,
Mchoro ukaujua, ni katuni
maridhiwa,
Unachokitegemea, kinaweza
kupotea!
Katika hii dunia, hupewa na
hutwaliwa,
Tayari unapokaa, hili utaling'amua,
Vyote aushi si nia, huja
vikajiondokea,
Unachokitegemea, kinaweza
kupotea!
Nipe ridhiko Jalia, kwa kuwa na
kutokuwa,
Ikawa kwa historia, utawa
ninaujua,
Ubora uliokuwa, ni kwa vyote
kuachia,
Unachokitegemea, kinaweza
kupotea!
Nisiwe wa kubomoa, patakapo
kukamua,
Jiwe kutokaribia, maziwa
halitatoa,
Katiti nilichopewa, nizidi
kuangalia,
Unachokitegemea, kinaweza
kupotea!
Nisiwe kung'ang'ania, pale
nisipotakiwa,
Kila anayechanua, thamani
hujikuzia,
Sina la kuongezea, siidanganyi dunia,
Unachokitegemea, kinaweza
kupotea!
Hapo nilipofikia, mbele
sintoendelea,
Yangu yamehasabiwa, zaidi
haitakuwa,
Mwalimu niliyekuwa, mwanafunzi
ninakuwa,
Unachokitegemea, kinaweza
kupotea!
Naenda tafuta njia, upenyoni
kupitia,
Nusura kuifichua, tunduni
iliokotiwa,
Mimi nikaichukua, mkononi kuitia,
Unachokitegemea, kinaweza
kupotea!
No comments:
Post a Comment