Monday, January 28, 2013

DUA ZETU HUWA DAWA...


Ninaianza tasua, kwa pazia kulitoa,

Jalali kaniridhia, shukrani ninatoa,

Siye niliyeanzia, karne zimeshatimia,

Dua zetu huwa dawa, uchamungu ukiwepo!

 

Viumbe hujifutua, uovu kuparamia,

Kama mipira ikawa, kudunda watarajia,

Ya watu huwazuzua, pabaya wakaingia,

Dua zetu huwa dawa, uchamungu ukiwepo!

 

Chini wanapoanzia, hudhania ni wakiwa,

Juu wakishafikia, pumzi huzitanua,

Fahari wakatamia, na kiburi kukitia,

Dua zetu huwa dawa, uchamungu ukiwepo!

 

Ujibari ukakua, ya Mola kuyachezea,

Visa mkasa ikawa, kwao ndio mazoea,

Ila siku hufikia, ukweli wakaujua,

Dua zetu huwa dawa, uchamungu ukiwepo!

 

Ila siku hufikia, ukweli wakaujua,

Hasa wanapoingia, imani iliyowakaa,

Mukubuli yao kuwa, yasiache kupokewa,

Dua zetu huwa dawa, uchamungu ukiwepo!

 

Uchamungu ukitua, meseji haitapotea,

Wenda inapotakiwa, kwa wakati kuingia,

Ikajionea dunia, ujumbe wakaujua,

Dua zetu huwa dawa, uchamungu ukiwepo!

 

Majina yetu bandia, kwa mengi sana twapwaya,

Vitabu twaviambaa, na dua kutozijua,

Nazo ibada kadhaa, zingine zinapotea,

Dua zetu huwa dawa, uchamungu ukiwepo!

 

Wakati umewadia, Yarabi kumrejelea,

yake tukasimamia, na hali njema ikawa,

Pamwe naye tutakuwa, bishara tukizitoa,

Dua zetu huwa dawa, uchamungu ukiwepo!

 

Nyakati zajifungua, sana wazi zinakuwa,

Gizani tuliyokuwa, mwanga sasa waingia,

Efemu kiifungua, chuoni unaingia,

Dua zetu huwa dawa, uchamungu ukiwepo!

 

Daraja unayetoa, hadh yetu angalia,

Shere wanaokusudia, mkengeni kuwatia,

Kamba umetupatia, tuwezeshe kutumia,

Dua zetu huwa dawa, uchamungu ukiwepo!

No comments: