Monday, January 28, 2013

Mtu akistuliwa....


Mola anayemridhia, hakosi kumgutua,

Kisa kinapotokea, akawa mwenye kujua,

Toba inayongojewa, si ile ya kutania,

Mtu akistuliwa, haachi kujitambua !

 

Hadharani hutokea, pasina kawa kutiwa,

Watu wakajionea, na ishara kuijua,

Yapo ya kuyachezea, mengine ni kujiua,

Mtu akistuliwa, haachi kujitambua !

 

Maumbile huacha, kazi yakajifanzia,

Vifua ikakunjua, hisia kuzielewa,

Kila asiyelaaniwa, tanzu akazitambua,

Mtu akistuliwa, haachi kujitambua !

 

Katika hii dunia, michache inabakia,

Anayejielewa, ajua la kuamua,

Anayezuzuliwa, hubakia kuchezea,

Mtu akistuliwa, haachi kujitambua !

 

Kinyago huchukuliwa, hadhiye anayopewa,

Mola akampatia, kambaye kuning'inia,

Akija kushtukia, wasaa unshawadia,

Mtu akistuliwa, haachi kujitambua !

 

Vidole huvitanua, alama akavitia,

Kisha vikakunjuliwa, ufahamu kuutia,

Kula mwenye kujaliwa, adhana akasikia,

Mtu akistuliwa, haachi kujitambua !

 

Kazi tunazojipea, daraja zinapungua,

Ila kwa kutokujua, bora tunazidhania,

Shetani akatuvaa, tukashindwa kuachia,

Mtu akistuliwa, haachi kujitambua !

 

Shehe Ali alijua, aweza kusimulia,

Baraza wakaikaa, na hali kuangalia,

Vingine vinavyotokea, vyawasuta wasokuwa,

Mtu akistuliwa, haachi kujitambua !

 

Namshukuru Jalia, fikra kunijalia,

Kuwaza na kuwazua, na wengine kumegea,

Uchoyo sikujaliwa, japo tajiri sijawa,

Mtu akistuliwa, haachi kujitambua !

No comments: