Saturday, January 26, 2013

KUOA UMPENDAYE


KATIKA yetu maisha, nasibu tunapangiwa,

Hauwezi kukatisha, wala kujiongezea,

Kadari huitimisha, liandikwalo likawa,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Joto wanaotupasha, na werevu kudhania,

Mioyo wakatingisha, na vifua kuinya,

Sio tunaoozeshwa, bahati huwakimbia,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Wasiotukorofisha, na presha kututia,

Daima wasiobisha, na uume kujitia,

Na wasiokutingisha, hadi ukachanganyikiwa,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Pingu wanaotuvisha, moyoni hawakuingia,

Ila muda ulitosha, kipindi kikafatia,

Ubishi unapoisha, miaka kuikimbia,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Wengine tuanozeshwa, kama vile twaolewa,

Ya wake kuyawezesha, yasipate kufifia,

Na ndugu wakikorofisha, ukajikuta pabaya,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Kuna wengine wazusha, mimba kukusingizia,

Wenye nazo wamechoshwa, wala hawakuridhia,

Si mtu wa kubisha, jukumu ukachukua,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Kunazo zisizo kesha, za mkeka twaambiwa,

Ulipojiburudisha, puani yakakutokea,

Kwao alishawachosha, mwanya wakiungojea,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Kuna za kujiimarisha, kipato kikatulia,

Wa mkwasi kumkosha, hata sura akipwaya,

Unatafuta maisha, mengine yatafatia,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Kuna wengine angusha, ujinga umewajaa,

Ila wajua zungusha, wanatia ukichaa,

Mkiyaanza masiha, hujiona umeliwa,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Kuna wa kuburudisha, si wa kukuongezea,

Kwalo hilo linatosha, kazi hapo yaishia,

Ukitaka jumlisha, kuzidisha na kutoa,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Kuna wa kubabaisha, jiko lipo kujitia,

Heshima kutokuisha, japo unaning'inia,

Na mikasa ya maisha, ndani huwa yabakia,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

 

Kuna wa kuelimisha kitu wasichokijua,

Ni wabishi wa kuchosha, hadi wanapoumia,

Hapo wakijirekebisha, jema waweza ambua,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Kuna wa kuneemesha, utajiri mkajua,

Mkayapenda maisha, na baraka kujaliwa,

Kama ni kuyarefusha, dua mkajiombea,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Kuna ya kukinaisha, nyumba ikawa balaa,

Ukataka yakomesha, katikati kuishia,

Ila ukajikausha, majukumu kutimia,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Katika yetu maisha, ndoa nyingi ni sanaa,

Twajaribu kuchekesha, na kukimbia udhia,

Tunatania watasha, ukweli kutokujua,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

 

Na DNA rabsha, siri inazifichua,

Katikati ya maisha, watu wakajichukia,

Walodhani wajitosha, wakakuta wapungua,

Kuoa umpendaye, huwa ni bahati kubwa !

No comments: