Changu kilipungukiwa, mbali ukakiambaa,
Wala hukukipitia, hali yake kuijua,
Ikawa kama wajua, kwako hayatatokea,
Changu ulinyanyapaa, kumbe yatakutokea ?
Mizimu ilichukia, kwa uliyoyanuia,
Kisha ikakutegea, pabaya kuangukia,
Somo hukulielewa, wala hutolielewa,
Changu ulinyanyapaa, kumbe yatakutokea ?
Kwa aliyekuchukulia, kama wake ulikuwa,
Wewe ukadhamiria, baki vile amekuwa,
Na wajibu kujitoa, nasaba ukaiavua,
Changu ulinyanyapaa, kumbe yatakutokea ?
Neno wakijisemea, Mungu anawasikia,
Wagonjwa waliokuwa, milango hufunguliwa,
Kalima kukubaliwa, malipo yako kupewa,
Changu ulinyanyapaa, kumbe yatakutokea ?
Laiti ungelijua, cheo usingetumia,
Juu ukajipitia, vya chini kuvichukia,
Udugu ukafumua, na nasaba kupangua,
Changu ulinyanyapaa, kumbe yatakutokea ?
Sasa yanakutokea, kwa uzito yanajaa,
Yaja yameshehenea, na vituko kuingia,
Dhihaka utadhania, mja inakuchezea,
Changu ulinyanyapaa, kumbe yatakutokea ?
Dua usipoijua, ibada kuikataa,
Nyuma kutorudia, wapi ulipoangukia,
Na tawba kufikia, bado shere itakuwa,
Changu ulinyanyapaa, kumbe yatakutokea ?
Nafuu ulishapewa, yako ukakimbilia,
Kuikusanya dunia, mfukoni kuitia,
Ila ninachohofia, yakukusanya dunia,
Changu ulinyanyapaa, kumbe yatakutokea ?
Suluhu ungeijua, amani ungelipew,
Ovyo umeidhania, na dharau kuitia,
Chambo umekichambua, na kitanzi kujitia,
Changu ulinyanyapaa, kumbe yatakutokea ?
Mbele nilitangulia, sio kwa kutojijua,
Mengi nikayaachia, na vichache kuchagua,
Kuna vingi vya dunia, kubeba huwa ukiwa,
Changu ulinyanyapaa, kumbe yatakutokea ?
Na hasa papa ukiwa, ukadhulumu dagaa,
Hatua itafikia, wenzi kukugeukia,
Ukajikuta mkiwa, huna cha kutumainia,
Changu ulinyanyapaa, kumbe yatakutokea ?
No comments:
Post a Comment