Monday, January 28, 2013

NDUGU WANAPOGOMBANA...


YAO kutoingilia, ni busara inakuwa,

Katika hii dunia, ndugu ni kuwaachia,

Yao wanayatambua, kwa dira na historia,

Ndugu wanapogombana, chukua jembe kalime!

 

Huna la kukadiria, katikati kuingia,

Udhia utajiria, pamwe aibu na haya,

Ila wakishatulia, 'siache wasalimia,

Ndugu wanapopatana, chukua kapu kavune!

 

Matusi yakitembea, na magumi kutambaa,

Nyumbani kwako ingia, jembe kwenda kuchukua,

Ujihimu kwelekea, shambani kujilimia,

Ndugu wanapogombana, chukua jembe kalime!

 

Kununa kukikiishia, tabasamu wakatoa,

Wakawa wakumbatia, kile walichochukia,

Kapu wende kutungua, kivuno kitakujia,

Ndugu wanapopatana, chukua kapu kavune!

 

Ngebe zinapotambaa, na mateke kutembea,

Inuka ulipokaa, kiserema kuchukua,

Matembele kuwania, uende kupalilia,

Ndugu wanapogombana, chukua jembe kalime!

 

Kicheko wakiangua, na hafla kuisikia,

Usiache karibia, na hodi kujigongea,

Sahau ikishaingia, huwa raha na furaha,

Ndugu wanapopatana, chukua kapu kavune!

 

Mbwa wakikubwekea, mguu ukate njia,

Mlango kutouvaa, usije ukavuliwa,

Yako ukakimbilia, hadi uishe wasaa,

Ndugu wanapogombana, chukua jembe kalime!

 

Nyimbo ukizikia, kama vile wamelewa,

Milango hufunguliwa, yote wazi inakuwa,

Ndani weza kuingia,nawe upate tanua,

Ndugu wanapopatana, chukua kapu kavune!

 

Bunduki ukisikia, usiwe wachungulia,

Waweza kutunguliwa, dirishani ukikaa,

Mvunguni kiingia, usalama  wanunua,

Ndugu wanapogombana, chukua jembe kalime!

 

Sherehe zikikolea, na mapambo yakajaa,

Jua yameamuliwa, na wewe kujititimua,

Kapu kutokuachia, tupu halitarejea,

Ndugu wanapopatana, chukua kapu kavune!

No comments: