Monday, January 28, 2013

WAPENZI KUCHUKIANA...


Wawili wanaopendana, wakaacha aminiana,

Wivu ukagandamana, na hofu ya kuumizana,

Hufariki muamana, iwe  kama ni laana,

Wajapokuchukizana, wapenzi huchukiana!

 

Huisha kuaminiana, watu wakahofiana,

Ikawa ni kuwindana, kwa usiku na mchana,

Raha wakawa hawana, ila ya kuchunguana,

Wajapokuchukizana, wapenzi huchukiana!

 

Zama waliokipatana, wakawa si waelewana,

Shere wameshachezana, mashavu wanuniana,

Na mioyo inapindana, ubaya kutakiana,

Wajapokuchukizana, wapenzi huchukiana!

 

Mahaba walopeana, sumu wakamwagiana,

Na nje kukashifiana,ya ndani kufichuana,

Siri pakawa hakuna, kila kitu ni bayana,

Wajapokuchukizana, wapenzi huchukiana!

 

Haya watatenguana, na udhu kukatazana,

Mbio wakatimuana, kwenda wasikotakikana,

Dunia ikawaona, sio watu wa maana,

Wajapokuchukizana, wapenzi huchukiana!

 

Sura watachafuana, zikawa tambo hazina,

Soni zikawa ni suna, paisna kuhifadhiana,

Wchache wakulingana, katu kutotokezana,

Wajapokuchukizana, wapenzi huchukiana!

 

Dira huharibiana, ziishe kupindana,

Mbele sasa kutoona, wawe wanaangaliana,

Huruma wakawa hana, na utu waozeana,

Wajapokuchukizana, wapenzi huchukiana!

 

Wakawa wa kushindana, ubaya kufanyiana,

Muafaka kuzozana, waaswapo kupatana,

Lengo wakawa hawana, wakabaki madubwana,

Wajapokuchukizana, wapenzi huchukiana!

 

Binadamu muungwana, haya anapoisana,

Na huruma kutona, kwa marefu na mapana,

Vingine ya binti suna, hayawani humuona,

Wajapokuchukizana, wapenzi huchukiana!

 

No comments: