Wednesday, January 16, 2013

MPENZI NIMPPENDAYE.....


Ni yule anijuaye, pasi kusema na yeye,

Na wala nisilitowe, awe aitikiaye,

Fikira zzangu zi naye, na zake yeye ninaye,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Ulimbowe si mwiliwe, ila  yake akiliye,

Mambo nizungumzaye, awe anielewaye,

Changamoto atoaye, ubora nisipunguwe,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Hali aielewaye, pasina kupiga yowe,

Dhiki avumiliaye, hata pale nimfinyawe,

Sio siri atoaye, hadi nje zifikie,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Mpenzi nimpendaye, ni yule ayeyukaye,

Ni laini akuwaye, siagi ni mithiliye,

Juani asibakiye, kote atiririkaye,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Mpenzi nimpandaye, si akakamaaye,

Hasira zisimwishiye, mwishowe avunjikaye,

Balaa impataye, awe achanganyikiwaye,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Ni yule atononokaye, si mfupa abakiye,

Mwenye siha kwa haliye, na ulaini ajae,'

Huyo si awachiaye, ila ajiondoaye,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Mpenzi nimpendaye, siye yule anunaye,

Mvimbisha  mashavuye, uhofu apasukaye,

Namtaka achekaye, kisha anitekenyaye,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Si anung'unikaye, na mimi nisisikie,

Ni dhahiri aliaye, limuumizalo nijue,

Nami nimsikiaye, na tatizo nitatue,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Mpenzi nimtakaye, ni yule nimtekenyae,

Saa zote achekeaye, hadi machozi atoe,

Kisha aniangalie, awe siye ashibaye,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Mpenzi nimpendaye, si kitu afichaye,

Yangu huwa yake yeye, na yake ni yangu miye,

Si anishtukizaye, matatizoni niishie,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Mpenzi nimakaye, ni yule aningojaye,

Subira asiishiwe, hadi manane ningie,

Mlango afunguaye, tabasamu linivae,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Si yule aamuaye, kwanza ni aulizaye,

Ukweli atafutae, si ya nje asikiaye,

Kisha nasi tuongee, tusilojua tujue,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Ni ukweli asemaye, uongo asiapiye,

Na hofu imjaaye, Mola asimghadhabikie,

Na kesho aigopaaye,  kiama kisimuumbue,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Mpenzi nimpendaye, huwa anidekezaye,

Machozi anifutaye, kwa laini mkonowe,

Kisha anibembelezaye, usingizi unijie,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Mpenzi nimpendaye, ni tunu nijaliwaye,

Kwa juu atokeaye, baraka ajaliwae,

Rehema anileteaye, heri nisipungukiwe,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Mpenzi nimpendaye, ni ahadi atunzaye,

Nadhiri atimizaye, kwa wakati 'sikawie,

Na hali aijuaye, ahadi asiitoe,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Huwa deni alipaye, mpenzi nimpendaye,

Si watu awarushaye, awe aaapiziwaye,

Kizazi yawafikie, hali hili wasijue,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Mpenzi nimtakaye, ni Mola anigaiye,

Si wa shetani nipewaye, pabaya aingizaye,

Majuto ayaletaye, dunia uichukie,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

Mpenzi nimpendaye, ni sababu nijaaye,

Kwanini nimpendaye, ila kubwa kuwa yeye,

Na kisha ni hai niwaye, kila nikiwapo naye,

Mpenzi nimtakaye, ni anijuliaye !

 

 

No comments: