Saturday, January 26, 2013

Aliyekutangulia



AJABU itatokea, wewe uliyefuatia,

Kidomo ukajitia, kwa alotangulia,

Uapizo kuutia, eti kwani wachukia,

Aliyekutangulia, waweza kumuapiza ?

 

Kama panao ubaya, mukubuli huwa dua,

Ila onyo ukipewa, watakiwa lichukua,

Vingine ukiamua, madhila unajitia,

Aliyekutangulia, waweza kumuapiza ?

 

Leo hutofikiria, hadi kesho ikiingia,

Ikawa umechelewa, yakufika yametua,

Na hii ndiyo dunia, ilivyo yake tabia,

Aliyekutangulia, waweza kumuapiza ?

 

Subira ukiijua, neno utalifatia,

Kisha ukalichimbua, na  mizizi kuing'oa,

Kama mhogo kuliwa, na sumu  kuondolewa,

Aliyekutangulia, waweza kumuapiza ?

 

Pepo katika dunia, huwa zina ya kuzua,

Hasa zikakurubia, tanga kwenda zisumbua,

Na vyombo vikaelea,  kule visikotakiwa,

Aliyekutangulia, waweza kumuapiza ?

 

Wengi yamewazuzua, bora wakayaachia,

Haraka kukimbilia, ziliokofika tamaa,

Wakija kujigundua, wakabakia kulia,

Aliyekutangulia, waweza kumuapiza ?

 

Vibaka kwenye dunia, daraja walishapewa,

Wa chini hutuhunia, wa juu twawachukua,

Pasina sisi kujua, mijitumwa kubakia,

Aliyekutangulia, waweza kumuapiza ?

 

Yao yakatengamaa, na yetu tukafulia,

Na saa ikiwadia, litafunguka pazia,

Nje tukajionea, sivyo ilivyotakiwa,

Aliyekutangulia, waweza kumuapiza ?

No comments: