Na nilikuangalia, na kutaka kukulea,
Mjinga kwako nikawa, na kubasi la kuvua,
Yangu uliyakataa, ya ngoroko kuchukua,
Dharau imekuponza, sasa wajidhalilisha!
Jeui ukajitia, na matusi kukujaa,
Dharau ukaivaa, na shanga kuivalia,
Nami kimya nikakaa, siku nikiingojea,
Dharau imekuponza, sasa wajidhalilisha!
Muda haukuchelewa, miaka ikafikia,
Uhuru ulipokuwa, na waoto wamekua,
Hukujua nangojea, ulidhani natania,
Dharau imekuponza, sasa wajidhalilisha!
Ulikuwa ni kichaa, mtu usiyesikia,
Yako kujifanyia, yasiyowapendezea,
Na laana kufukua, na wana kuwatupia,
Dharau imekuponza, sasa wajidhalilisha!
Mapenzi hukujaliwa, ila wabeba sanaa,
Kila kitu kujitia, wajua usiyejua,
Wengi wakakushangaa, ujinga uliovaa,
Dharau imekuponza, sasa wajidhalilisha!
Juzuu kukazania, sasa unattakiwa,
Sura Na'ba kuijua, dua ukaiombea,
Maradhi kukupungua, kichwani yalokujaa,
Dharau imekuponza, sasa wajidhalilisha!
Na jeneza kuzuia, wana lisije chukua,
Wazee wako yafaa, kinga kuwaulizia,
Upuuzi uliotoa, madhara kutotokea,
Dharau imekuponza, sasa wajidhalilisha!
Ni mpweke nitakuwa, ila kensa naitoa,
Pengine nitafikiria, madeni ukilipiwa,
Nyumbani ukarejea, mama wa nyumbani kuwa,
Dharau imekuponza, sasa wajidhalilisha!
Biashara nakataa, marufuku kuijua,
Ila vitu kuandaa, nyumbani unapokuwa,
Na mikopo kuchukua, si ruhusa nakwambia,
Dharau imekuponza, sasa wajidhalilisha!
Wataka waharibia, wana wangali wakua,
Msingi kumalizia, chini wote kuishia,
Hakika wakosa haya, kisirani umekuwa,
Dharau imekuponza, sasa wajidhalilisha!
Na jeuri wajitia, kujifanya waonewa,
Mwisho umeshafikia, ukweli tunaujua,
Wengi umewaibia, siku zote wanalia,
Dharau imekuponza, sasa wajidhalilisha!
Nakuomba angukia, ndugu kukusaidia,
Mikopo uliyochukua, na wizi ulokuwa,
Madeni kukulipia, salama upate kuwa,
Dharau imekuponza, sasa wajidhalilisha!
No comments:
Post a Comment