Saturday, February 25, 2012

Walioshindwa mbinu


Mbinu walioishiwa, wepesi kukimbilia,

Fujo kuzichochea, wavune yanayowafaa,

Ukubwa kuutetea, japo waisha raia,

Walioshindwa mbinu, mikakati na fikra:

Mabavu huyatumia!

Ni watu wa kuteua, watu wasiowafaa,

Yao waangalia, si ya wengi yakawa,

Ni laana tumeachiwa, bado tunaing'ang'ania,

Walioshindwa mbinu, mikakati na fikra:

Mabavu huyatumia!

Enzi za kutofikiria, ukingoni zafikia,

Watu wataulizia, hata yale yasokuwa,

Na wajibu kuwatia, wajifanyao wajua,

Walioshindwa mbinu, mikakati na fikra:

Mabavu huyatumia!

Majoho watawavua, yafichyo kuishiwa,

Ujinga wakawaachia, na wengine kuchagua,

Pasiwe wa kubakia, na mtu anayetumiwa,

Walioshindwa mbinu, mikakati na fikra:

Mabavu huyatumia!

No comments: