Saturday, February 25, 2012

Unapojenga chuki

Mwaziogopa zahama, ndani mnatufatia,

Nani aliyewatuma, au kisasi mwatukua,

Nahisi kuna nakama, hawajui wasojua,

Unapojenga chuki, kwa polisi na raia:

Taifa unaliua,

Umoja unaambaa,

Na amani yapotea!

Zana mnazozifuma, vitani zilitakiwa,

Au migodi kuchuma, hicho kinachoibiwa,

Sio kuutesa umma, na uyatima kwingia,

Unapojenga chuki, kwa polisi na raia:

Taifa unaliua,

Umoja unaambaa,

Na amani yapotea!

Mwaturudisha nyuma, juu mliotangulia,

Na busara na hekima, yawa kama isokuwa,

Ni mashaka na tuhuma, nyuma yanawafatia,

Unapojenga chuki, kwa polisi na raia:

Taifa unaliua,

Umoja unaambaa,

Na amani yapotea!

Mambo yataka kalima, si magomvi kuyazua,

Utu usio heshima, haikubali dunia,

Hata mtumie vyuma, haki itapiganiwa,

Unapojenga chuki, kwa polisi na raia:

Taifa unaliua,

Umoja unaambaa,

Na amani yapotea!

Mwatia watu ulema, ndani waliotulia,

Na uongo kuusema, deraya wanavamia,

Hachagui la kusema, muongo alolaaniwa,

Unapojenga chuki, kwa polisi na raia:

Taifa unaliua,

Umoja unaambaa,

Na amani yapotea!

Nchi yataka adhama, watu waliojaliwa,

Wenye kuwa roho njema, na uhai kuulea,

Si wenye kuwasakama, hatia wasiokuwa,

Unapojenga chuki, kwa polisi na raia:

Taifa unaliua,

Umoja unaambaa,

Na amani yapotea!

Mkoloni anasema, mbinu zetumia,

Dhidi ya kwao umma, kama tulivyoanzia,

Ni ipi yao heshima, kulikoni tulokuwa?

Unapojenga chuki, kwa polisi na raia:

Taifa unaliua,

Umoja unaambaa,

Na amani yapotea!

Weupe watusakama, weusi wameingia,

Feli na zao kalima, yale yale yamekuwa,

Dunia hii sinema, na mcheza utamjua!

Unapojenga chuki, kwa polisi na raia:

Taifa unaliua,

Umoja unaambaa,

Na amani yapotea!

Mola wetu muadhama, tabia aichukia,

Na wasio na hekima, kwenu kujipalilia,

Wakidai mwendo nyuma, bei yao twaijua,

Unapojenga chuki, kwa polisi na raia:

Taifa unaliua,

Umoja unaambaa,

Na amani yapotea!

No comments: