Tuesday, February 14, 2012

Swali la wakati wetu


Nchi inadidimia, wakubwa waifagia,

Juu wataka bakia, hata ngazi pasokuwa,

Na sakafu yatitia, wao wanashindilia,

Swali la wakati wetu, posho au bila posho ?

Haya wasioijua, wataka kuazimia,

Bila ya kuzingatia, kilio tunacholia,

Yatima tumebakia, hakuna wa kutufaa,

Swali la wakati wetu, posho au bila posho ?

Wakubwa kulia njaa, uchuro huu balaa,

Hali wadogo wajua, matumbo wanapepea,

Hamjui mwenye njaa, wa shibe anaaminia,

Swali la wakati wetu, posho au bila posho ?

Mizani wakitumia, daima imepungua,

Nchi walipoanzia, mbele watatu adawa,

Hamsini kutimia, ni maadui kadhaa!

Swali la wakati wetu, posho au bila posho ?

Kama hamjautoa, umaskini ulokuwa,

Vipi mnaongezewa, msichokwishatuongezea?

Ila njaa na kut'ua, wenyewe mkabakia?

Swali la wakati wetu, posho au bila posho ?

Kazi mkjifanyia, bila kitu kwongezea,

Haifai kujapewa, juu chochote kikiwa,

Wajibu haujatimia, hapo mtatuibia,

Swali la wakati wetu, posho au bila posho ?

Wabunge mnatakiwa, jambo hili kulijua,

Watumishi nao pia, nchi wanaotumikia,

Posho mliyokipewa, sasa ya kuondolewa,

Swali la wakati wetu, posho au bila posho ?

Ila mtakapoyazua, wananchi yakawafa,

Kipato kuwaongezea, na shida kuwaondolea,

Bonasi mtapokea, tena kubwa zilokuwa,

Swali la wakati wetu, posho au bila posho ?

Februari 1, 2012

Dar es Salaam

No comments: