Monday, February 6, 2012

Sisi twatibiwa nje

Wengine nawashangaa, lawama wanazotoa,
Laiti wangelijua, hili wangelifukia,
Siye tumeandikiwa, nyie bado andikiwa,
Sisi twatibiwa nje, hospitali za Uswazi:
Zatuhusu kitu gani?

Wa kushoto na kulia, India tunaingia,
Au Sauzi kuridhia, Wazulu kuwaamkua,
Nyie hamjafikia, walal hamtafikia,
Sisi twatibiwa nje, hospitali za Uswazi:
Zinatuhusu kitu gani?

Wa chini haitokuwa, juu akaruhusiwa,
Na juu hukataliwa, aende chini kukaa,
Hii ni kweli ya dunia, hata pepo yatambua,
Sisi twatibiwa nje, hospitali za Uswazi:
Zinatuhusu kitu gani?

Msije mkajitia, kwa msiyo yaelewa,
Vibaya mtaumia, na mengi mkazushiwa,
Na za wakubwa dawa, kwenu sumu zitakuwa,
Sisi twatibiwa nje, hospitali za Uswazi:
Zinatuhusu kitu gani?

Usawa hautokuwa, katika hii dunia,
Angalia pepo pia, wa peponi huingia,
Kahaliika nao pia, wa motoni wakubaliwa,
Sisi twatibiwa nje, hospitali za Uswazi:
Zinatuhusu kitu gani?

Mila zetu zakataa, vingine ni kujikwaa,
Maisha ni kuchagua, chagua kuendelea,
Kuiga hakutokufaa, kwani waweza lemaa,
Sisi twatibiwa nje, hospitali za Uswazi:
Zinatuhusu kitu gani?

Februari 8, 2012,
Dar es Salaam.

No comments: