Tuesday, February 14, 2012

Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !


Bahati wasiopewa, hupata kikapotea,

Yalo mema huitiwa, nao wakayakimbia,

Pepo hutengenezewa, moto wakauchagua,

Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Asali huiambaa, shubiri wakachagua,

Neema huikemea, balaa wakaridhia,

Nusura huikimbia, maasi wakaingia,

Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Chumvi huichagua, sukari ikitakiwa,

Maji huyazidishia, ukavu unapotakiwa,

Gia ya nyuma hutia, ya mbele ikitakiwa,

Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Chini hujifukia, juu wanapotakiwa,

Gizani hukomelea, nuru nje imejaa,

Milioni hutumia, wakati yatosha mia,

Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Uoni huwapungua, uongo ukiwavaa,

Ya kweli huyakataa, uzaini kuridhia,

Juto mjukuu huwa, Joti wakamuachia,

Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Januari 29, 2012

Dar es Salaam

No comments: