Saturday, February 25, 2012

Starehe gani hii ?


Kila mtu ashangaa, dhiki waikimbilia,

Wengi wanavyodhania, pengine umechezewa,

Kulogwa inshakuwa, huu nusu ukichaa,

Starehe gani hii, dhiki kuikimbilia ?

Si bure umechezewa, au mzazi kachukia,

Mema unayotendewa, kwako ubaya inkuwa?

Wengine waililia, nafasi uliyopewa,

Starehe gani hii, dhiki kuikimbilia ?

Uhuru umegaiwa, wewe waudhihakia,

Unaibeza tabia, ya ulua wa kufaa,

Na uchafu wautwaa, mwilini kujimwagiwa,

Starehe gani hii, dhiki kuikimbilia ?

Huu kama ukichaa, naona ilivyokuwa,

Kila siku ikiingia, hali huwa kote mbaya,

Watu wanaulizia, kanyimwa na kupagawa?

Starehe gani hii, dhiki kuikimbilia ?

Wabaya washangilia, zuzu kusesembuliwa,

Raha waitamania, ije kuwaangukia,

Kila wakikazania, kofuli bado yatiwa,

Starehe gani hii, dhiki kuikimbilia ?

Lango langu kufungua, haijawa, nanuia,

Hadi akitokea, malaika atembea,

Urulaini radhia, duniani akajaa,

Starehe gani hii, dhiki kuikimbilia ?

Mazuri wayaachia, mabaya wang'ang'ania,

Nini kinakuzuzua, bado hatujakijua,

Kila pembe twaulizia, majibu hatujapewa,

Starehe gani hii, dhiki kuikimbilia ?

Mtaji umeitwaa, nani kukusaidia,

Wazazi nini kupewa, hali pato umeua?

Wallahi nakusikitia, ninatamani kulia,

Starehe gani hii, dhiki kuikimbilia ?

Raha uliidhania, nje utajiokotea,

Ndani ukapachukia, na wa ndani kuwa udhia,

Laiti ungelijua, ndani ungejiangalia,

Starehe gani hii, dhiki kuikimbilia ?

No comments: