Monday, February 6, 2012

Uheshimiwa msikitini ?

Ya msikiti si yenu, wakubwa mliokuwa,
Hapa si pahali penu, si siasa ni daawa,
Zichukueni fununu, kwingine kuhamishia,
Uheshimiwa msikitini,
Hivi Mungu twamchezaea?

Kanuni tunazijua, ibada yake sheria,
Wa kwanza kutangulai,safu mbele akakaa,
Nyuma wanaoingia, lazima nyuma kukaa,
Uheshimiwa msikitini,
Hivi Mungu twamchezaea?

Dini mnatangazia, siasa haitofaa,
Mseti kujipikia, chakula kibichi huwa,
Nasi tunawambia,sera zenu si dua,
Uheshimiwa msikitini,
Hivi Mungu twamchezaea?

Protokoli ya dua, na ibada twaijua,
Ya siasa ilokuwa, kwingine kuitumia,
Heshima wa kwanza kuwa, wengine wakafuatia,
Uheshimiwa msikitini,
Hivi Mungu twamchezaea?

Nani anayemjua, mtukufu alokuwa,
Aliyekwishachaguliwa, na pepo keshaipewa,
Yumkini hatokuwa, mkubwa tunayemjua,
Uheshimiwa msikitini,
Hivi Mungu twamchezaea?

Huyo aweza akawa, mbaya anayechukiwa,
Mbingu zimemkataa, kwa dhambi anazochukua,
Hasira mkaivaa, baa kuvurumishiwa,
Uheshimiwa msikitini,
Hivi Mungu twamchezaea?

Na uchafu ulokua, patakatifu kukaa,
Malaika wakapaa, na nje kuondokea,
Uoza kuukataa, hewa unavyochafua,
Uheshimiwa msikitini,
Hivi Mungu twamchezaea?

Viongozi mwatakiwa, haya kuyafafanua,
Msije mkaichezea, nyumba ya Mungu ilokuwa,
Kwa kutaka jinyanyua, migongoni kupitia,
Uheshimiwa msikitini,
Hivi Mungu twamchezaea?

Ukubwa mkiwania, hapa si pa kujipatia,
Nendeni kunakofaa, ya kwenu kuhangaikia,
Waumini twakataa, si ibadani yakawa,
Uheshimiwa msikitini,
Hivi Mungu twamchezaea?

Februari 8. 2012,
Dar es Salaam.

No comments: