Saturday, February 25, 2012

Kumpanda mume la'na, na sasa unayaona!


Na nilikuangalia, na kutaka kukulea,

Mjinga kwako nikawa, na kubasi la kwogea,

Yangu uliyakataa, ya ngoroko kuchukua,

Kumpanda mume la'na, na sasa unayaona!

Jeui ukajitia, na matusi kukujaa,

Dharau ukaivaa, na shanga kuivalia,

Nami kimya nikakaa, siku nikiingojea,

Kumpanda mume la'na, na sasa unayaona!

Muda haukuchelewa, miaka ikafikia,

Uhuru ulipokuwa, na waoto wamekua,

Hukujua nangojea, ulidhani natania,

Kumpanda mume la'na, na sasa unayaona!

Ulikuwa ni kichaa, mtu usiyesikia,

Yako kujifanyia, yasiyowapendezea,

Na laana kufukua, na wana kuwatupia,

Kumpanda mume la'na, na sasa unayaona!

Mapenzi hukujaliwa, ila wabeba sanaa,

Kila kitu kujitia, wajua usiyejua,

Wengi wakakushangaa, ujinga uliovaa,

Kumpanda mume la'na, na sasa unayaona!

Juzuu kukazania, sasa unattakiwa,

Sura Na'ba kuijua, dua ukaiombea,

Maradhi kukupungua, kichwani yalokujaa,

Kumpanda mume la'na, na sasa unayaona!

Na jeneza kuzuia, wana lisije chukua,

Wazee wako yafaa, kinga kuwaulizia,

Upuuzi uliotoa, madhara kutotokea,

Kumpanda mume la'na, na sasa unayaona!

Ni mpweke nitakuwa, ila kensa naitoa,

Pengine nitafikiria, madeni ukilipiwa,

Nyumbani ukarejea, mama wa nyumbani kuwa,

Kumpanda mume la'na, na sasa unayaona!

Biashara nakataa, marufuku kuijua,

Ila vitu kuandaa, nyumbani unapokuwa,

Na mikopo kuchukua, si ruhusa nakwambia,

Kumpanda mume la'na, na sasa unayaona!

Wataka waharibia, wana wangali wakua,

Msingi kumalizia, chini wote kuishia,

Hakika wakosa haya, kisirani umekuwa,

Kumpanda mume la'na, na sasa unayaona!

Na jeuri wajitia, kujifanya waonewa,

Mwisho umeshafikia, ukweli tunaujua,

Wengi umewaibia, siku zote wanalia,

Kumpanda mume la'na, na sasa unayaona!

Nakuomba angukia, ndugu kukusaidia,

Mikopo uliyochukua, na wizi ulokuwa,

Madeni kukulipia, salama upate kuwa,

Kumpanda mume la'na, na sasa unayaona!

No comments: