Tuesday, February 14, 2012

Uonevu ukizidi


BASHIRI macho hafungi, na huona kila jambo,

Msije kula mirungi, muone yasiyo tambo,

Ya mja hayamchengi, kwa sauti au wimbo,

Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Kinyonga kwake haringi, ndiye aliyempa umbo,

Humbadili kwa rangi, adawa kukwepa mkumbo,

Na kwa mapozi ni kingi, ashinda hata mgambo,

Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Viumbe walio wengi, ni wadogo kwa maumbo,

Na si watu wa mitungi, wala kwa wingi mapambo,

Hutafuta la msingi, mengine kwao vijambo,

Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Lakini mlangilangi, yao yaendayo kombo,

Hutafuta kama nungwi, yaumizayo matumbo,

Kunao wavuta bangi, wajifanyao ni Rambo,

Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Nao wenye mali nyingi, huwatumia mgambo,

Hawana chao kichungi, haki kuwa mtarimbo,

Watakayo ni shilingi, wengine kula vikumbo,

Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Tamaa hawajivungi, hukaa nawe kitambo,

Hutumia nguvu nyingi, kuzikuza zao tambo,

Hata wenye fungu jingi, huzama kwenye mkumbo,

Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Omwami na kina mangi, wanayaguna mafumbo,

Kadhalika na wasangi, na watani zao Rombo,

Hukiondoa kigungi, hata wakenda Urambo,

Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Mwana muulize Dingi, kama naye ana jambo,

Nawe uwe ni mchungi, kunusuru lako tumbo,

Na ukaushe matangi, kwa dhuluma yake chambo,

Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Januari 29, 2012

Dar es Salaam

No comments: