Tuesday, February 14, 2012

Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !


Mariamu sikiliza, ushauri nakwambia,

Usijefanya kuiza, ukaja kuyajutia,

Mkataa ukewenza, sinamume hujakua,

Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Amri inaeleza, weye unaitania,

Mwenyewe wajimaliza, kesho kujiharibia,

Dini unaipuuza, kwa kukosa zingatia,

Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Ndoa hukupa makazi, kwa wazazi unakaa?

Ndoa hukupa malezi, mumeo kukuangalia,

Ndoa hukupa malazzi, libasi ukaijua,

Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Ndoa hukupa malazzi, libasi ukaijua,

Mwenzio kuwa pumzi, nawewe ukapumua,

Kitulizo chenye enzi, kila mmoja akawa,

Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Mola ukimkabidhi, moyoni yaliyokuwa,

Hakika huyahifadhi, nawewe ukajaliwa,

Akakupa wema wenzi, ndoa mkawa wabia,

Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Atakupa wema wenzi, ndoa mkawa wabia,

Mkawa wasaidizi, nyumba kuiangalia,

Mkapewa na uzazi, udugu mkachangia,

Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Na yakiwepo maradhi, wote kujihudumia,

Mkazigawa na kazi, na zamu kujipangia,

Pasiwe na kizuizi, kwa feli kuziamua,

Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Ni chuo chenye ujuzi, mengi mtakujayajua,

Na pawapo yake radhi, Mola huyaafikia,

Mkaipanda ngazi, wote peponi kwingia,

Wakataa ukewenza, utaitwa mumesina !

Januari 29, 2012

Dar es Salaam

No comments: