Uongo linavyojaa, hakika hii balaa,
Huzua wanayozua, na umbeya kuutia,
Hakuna la kuzingatia, uchama tupu lajaa,
Redio ya chama jaa, ukisikiza kinyaa!
Linachangia kuua, haki pia na usawa,
Wakubwa lawatetea, hata watu wakiuua,
Tumeona Tunisia, twangojea Tanzania,
Redio ya chama jaa, ukisikiza kinyaa!
Mamluki huchukua, uandishi kuachiwa,
Na kada mtarajiwa, mhariri anakuwa,
Kazi yao ni umbeya, na ukweli kukataaa,
Redio ya chama jaa, ukisikiza kinyaa!
Huwa kama changudoa, jinsi wanavyotumia,
Haya huwakimbia, na aibu kuwaambaa,
Wanenalo ni nazaa, si watu wa kusikiwa,
Redio ya chama jaa, ukisikiza kinyaa!
Maneno wanavyojua, kuunda na kutumia,
Uongo yaliyojaa, akili hukupindua,
Anzali kama ukiwa, rahisi kuzainiwa,
Redio ya chama jaa, ukisikiza kinyaa!
Na wanademokrasia, watu hawa wawajua,
Watawaliwa na njaa, umalaya kuridhia,
Hukumu yawangojea, kiyama kikiingia,
Redio ya chama jaa, ukisikiza kinyaa!
Unafiki wamejaa, wakafikia kuua,
Watu kuwasingizia, hata wasiyotambua,
Kupatiliza yafaa, na laana kuwaombea,
Redio ya chama jaa, ukisikiza kinyaa!
Yarabi nakulilia, jehanamu kuambaa,
Vigogo kutonitumia, ukweli nikachuuzia,
Sauti niliyopewa, uongo kutoridhia,
Redio ya chama jaa, ukisikiza kinyaa!
Friday, February 10, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment