Saturday, February 25, 2012

Umeme unapozima


Kwenye nchi ya madoa, rangi tusiyoyajua,

Na amri za kuua, wadhani hawajaua,

Na yatakiwayo kuwa, yasiwe yenye kukua,

Umeme unapozima, na giza likaenea:

Mwangaza hunifunua,

Utunzi nikaingia,

Hadi adhana ikawa!

Ukuu wanaochukua, wasiwe pakuanzia,

Na wanaoyachimbua, wakadhani walimia,

Huwa nchi ya wafukua, kuzikwa kwao haijawa,

Umeme unapozima, na giza likaenea:

Mwangaza hunifunua,

Utunzi nikaingia,

Hadi adhana ikawa!

Ndipo saa wazijua, kizani kutususia,

Mengi yananipitia, pembeni nilipokaa,

Wasiojua wajua, ndiyo nchi imekuwa,

Umeme unapozima, na giza likaenea:

Mwangaza hunifunua,

Utunzi nikaingia,

Hadi adhana ikawa!

Hakuna wa kutumiwa, wote wataka tumia,

Kuvuna washangilia, kupanda wanakataa,

Wachache hupalilia, nao mimea hung'oa,

Umeme unapozima, na giza likaenea:

Mwangaza hunifunua,

Utunzi nikaingia,

Hadi adhana ikawa!

Nchi ya wasiojijua, na kwendako wapotea,

Taifa lisilojifua, kutakata haijawa,

Na uchafu waujua, tena wanautumia,

Umeme unapozima, na giza likaenea:

Mwangaza hunifunua,

Utunzi nikaingia,

Hadi adhana ikawa!

Watu wa kusaidiwa, wasiojisaidia,

Nchi yenye kununua, chake isichokizaa,

Ni nchi ya kulaniwa, mbele haitoendelea,

Umeme unapozima, na giza likaenea:

Mwangaza hunifunua,

Utunzi nikaingia,

Hadi adhana ikawa!

Nchi ya viguu na njia, haiwezi kutulia,

Yao wasiotatua, ya wengine wakavaa,

Ni ya kusikitikiya, na tena kuhurumiwa,

Umeme unapozima, na giza likaenea:

Mwangaza hunifunua,

Utunzi nikaingia,

Hadi adhana ikawa!

Ndio ninafurahia, umeme ukisinzia,

Huamka na kuzua, visa vya kuhadithia,

Kizazi kitachokuwa, haya kuja yaambaa,

Umeme unapozima, na giza likaenea:

Mwangaza hunifunua,

Utunzi nikaingia,

Hadi adhana ikawa!

No comments: