Na nilikuangalia, na kutaka kukulea,
Mjinga kwako nikawa, na kubasi la kuvua,
Yangu uliyakataa, ya ngoroko kuchukua,
Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?
Jeui ukajitia, na matusi kukujaa,
Dharau ukaivaa, na shanga kuivalia,
Nami kimya nikakaa, siku nikiingojea,
Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?
Muda haukuchelewa, miaka ikafikia,
Uhuru ulipokuwa, na waoto wamekua,
Hukujua nangojea, ulidhani natania,
Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?
Ulikuwa ni kichaa, mtu usiyesikia,
Yako kujifanyia, yasiyowapendezea,
Na laana kufukua, na wana kuwatupia,
Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?
Mapenzi hukujaliwa, ila wabeba sanaa,
Kila kitu kujitia, wajua usiyejua,
Wengi wakakushangaa, ujinga uliovaa,
Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?
Juzuu kukazania, sasa unattakiwa,
Sura Na'ba kuijua, dua ukaiombea,
Maradhi kukupungua, kichwani yalokujaa,
Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?
Na jeneza kuzuia, wana lisije chukua,
Wazee wako yafaa, kinga kuwaulizia,
Upuuzi uliotoa, madhara kutotokea,
Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?
Ni mpweke nitakuwa, ila kensa naitoa,
Pengine nitafikiria, madeni ukilipiwa,
Nyumbani ukarejea, mama wa nyumbani kuwa,
Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?
Biashara nakataa, marufuku kuijua,
Ila vitu kuandaa, nyumbani unapokuwa,
Na mikopo kuchukua, si ruhusa nakwambia,
Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?
Wataka waharibia, wana wangali wakua,
Msingi kumalizia, chini wote kuishia,
Hakika wakosa haya, kisirani umekuwa,
Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?
Na jeuri wajitia, kujifanya waonewa,
Mwisho umeshafikia, ukweli tunaujua,
Wengi umewaibia, siku zote wanalia,
Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?
Nakuomba angukia, ndugu kukusaidia,
Mikopo uliyochukua, na wizi ulokuwa,
Madeni kukulipia, salama upate kuwa,
Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?
No comments:
Post a Comment