Saturday, February 25, 2012

Kiburi kimekuponza,

Na nilikuangalia, na kutaka kukulea,

Mjinga kwako nikawa, na kubasi la kuvua,

Yangu uliyakataa, ya ngoroko kuchukua,

Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?

Jeui ukajitia, na matusi kukujaa,

Dharau ukaivaa, na shanga kuivalia,

Nami kimya nikakaa, siku nikiingojea,

Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?

Muda haukuchelewa, miaka ikafikia,

Uhuru ulipokuwa, na waoto wamekua,

Hukujua nangojea, ulidhani natania,

Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?

Ulikuwa ni kichaa, mtu usiyesikia,

Yako kujifanyia, yasiyowapendezea,

Na laana kufukua, na wana kuwatupia,

Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?

Mapenzi hukujaliwa, ila wabeba sanaa,

Kila kitu kujitia, wajua usiyejua,

Wengi wakakushangaa, ujinga uliovaa,

Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?

Juzuu kukazania, sasa unattakiwa,

Sura Na'ba kuijua, dua ukaiombea,

Maradhi kukupungua, kichwani yalokujaa,

Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?

Na jeneza kuzuia, wana lisije chukua,

Wazee wako yafaa, kinga kuwaulizia,

Upuuzi uliotoa, madhara kutotokea,

Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?

Ni mpweke nitakuwa, ila kensa naitoa,

Pengine nitafikiria, madeni ukilipiwa,

Nyumbani ukarejea, mama wa nyumbani kuwa,

Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?

Biashara nakataa, marufuku kuijua,

Ila vitu kuandaa, nyumbani unapokuwa,

Na mikopo kuchukua, si ruhusa nakwambia,

Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?

Wataka waharibia, wana wangali wakua,

Msingi kumalizia, chini wote kuishia,

Hakika wakosa haya, kisirani umekuwa,

Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?

Na jeuri wajitia, kujifanya waonewa,

Mwisho umeshafikia, ukweli tunaujua,

Wengi umewaibia, siku zote wanalia,

Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?

Nakuomba angukia, ndugu kukusaidia,

Mikopo uliyochukua, na wizi ulokuwa,

Madeni kukulipia, salama upate kuwa,

Kiburi kimekuponza, mbona sasa unalia ?

No comments: