Saturday, February 25, 2012

Kuiga mambo ya watu

Akili hukutumia, ingwa umejaliwa,

Bahati ukachezea, chooni ulipokuwa,

Shilingi kutumbukia, vyote vimeshapotea,

Kufata watu wa nje, wa ndani ukawabeza:

Nyongo yakutumbukia!

Ya mme hukusikia, kiburi ukajitia,

Na jeuri ukawa, kila alipokuongoa,

Heri ukaikataa, na shari kukurubia,

Kufata watu wa nje, wa ndani ukawabeza:

Nyongo yakutumbukia!

Wa nje kuwaendea, shirika kujifanyia,

Na waganga kuzoea, ushirikina kujaa,

Mkawa mwachanganyikiwa, mwazidi potea njia,

Kufata watu wa nje, wa ndani ukawabeza:

Nyongo yakutumbukia!

Wakowapi walokua, kila siku wasifia,

Kidume uliyekuwa, mume chini yako kawa,

Kumbe akuhesabia, siku yako kufikia,

Kufata watu wa nje, wa ndani ukawabeza:

Nyongo yakutumbukia!

Sura ulipuuzia, ila dini wajitia,

Kurani hukuijua, ubishi ulikujaa,

Na ulichoambulia, mwenyewe unakijua,

Kufata watu wa nje, wa ndani ukawabeza:

Nyongo yakutumbukia!

Un afiki kujitia, na uswalihina pia,

Kumbe nyoka ulikua, kichinichini wajia,

Kutuchoma kuamua, nyumbani tulokaa,

Kufata watu wa nje, wa ndani ukawabeza:

Nyongo yakutumbukia!

Dunia yakuumbua, mwanamke wa balaa,

Haya hukuitambua, nani kukuangalia,

Mola ukimrudia, pengine kukuafua,

Kufata watu wa nje, wa ndani ukawabeza:

Nyongo yakutumbukia!

Ushirikina kimbia, au unaangamia,

Na mume kumwangukia, ndiyo dawa itakuwa,

Vinginevyo twachomoa, akhera mbali pia kuwa,

Kufata watu wa nje, wa ndani ukawabeza:

Nyongo yakutumbukia!

Dhuluma kujifanyia, na urushi kuujua,

Sumu yake hukujua, wanao itawavaa,

Wajukuu nao pia, usipowarejeshea,

Kufata watu wa nje, wa ndani ukawabeza:

Nyongo yakutumbukia!

Rahma ungelikuwa, haya yasingetokea,

Ila kwa kukosa neema, ulizaliwa Rehema,

Tubu kisha ungamia,

Kufata watu wa nje, wa ndani ukawabeza:

Nyongo yakutumbukia!

No comments: